Header Ads

Serikali yazikumbusha Kampuni za Mawasiliano Kujisajili Soko la Hisa

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa, amezitaka Kampuni za Mawasiliano kukamilisha taratibu za usajili katika Soko la Hisa la Dar es Salaam kwa kuuza asilimia 25 ya hisa zote kadri ya Sheria ya Masoko ya Mitaji na Dhamana inavyoelekeza mwishoni mwa mwaka huu.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Prof. Mbarawa ametaja kampuni hizo kuwa ni zile zenye leseni za mawasiliano zilizotolewa kabla ya tarehe 1 Julai 2016 kwa ajili ya Miundombinu ya Mawasiliano, Huduma za Mawasiliano, na Huduma za Matumizi.

“Watoa huduma wote wa Mawasiliano wajisajili na kuuza hisa zao kwa wananchi ndani ya mwezi wa Disemba”, amesema Waziri Prof. Mbarawa.

Ameongeza kuwa kwa Kampuni zilizopata leseni baada ya tarehe mosi Julai, 2016 watatakiwa kutimiza sharti hilo la kisheria kwa kipindi kisichozidi miaka miwili tangu kusajiliwa.

Waziri Prof. Mbarawa amesisitiza kuwa Kampuni zitakazokiuka Sheria hiyo zitachukuliwa hatua za kisheria kupitia kifungu cha 21 (C) cha EPOCA, 2010.


Aidha, amewataka wananchi kutumia fursa hiyo kununua hisa hizo na kuwa sehemu ya wamiliki wa makampuni ya Mawasiliano ili kuongeza kipato na kushiriki katika maamuzi ya kampuni hizo.

No comments

Powered by Blogger.