Header Ads

Naibu Waziri SELEMAN JAFO aagiza Wazazi Wasiopeleka watoto Shule Wawajibishwe

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) Selemani Jafo akitoka kukagua ujenzi wa choo cha walimu katika shule ya msingi Chang’ombe ‘B’ wakati wa ziara yake aliyoifanya katika kata ya Chang’ombe manispaa ya Dodoma.

Naibu Waziri wa Nchi  Ofisi ya Rais  Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Selemani Jafo  akizungumza mara baada ya kumalizia ziara yake kwa kukagua miundo mbinu ya majitaka katika shule ya msingi Chadulu na kutoa maagizo kwa wakuu wa wilaya nchini.

      ................................................


Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(Tamisemi), Selemani Jafo amewaagiza Wakuu wa wilaya nchini kuhakikisha wanafunzi waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu wanakwenda kuanza shule huku akiwasisitiza wazazi watakaoshindwa kuwapeleka shule watoto hao wachukuliwe hatua za kisheria.



Jafo ametoa agizo hilo leo alipofanya ziara ya kukagua miundombinu mbalimbali katika shule za msingi, Chadulu, Chang’ombe A na B, Manispaa ya Dodoma.



Katika ziara yake ya kukagua maagizo aliyoyatoa kwenye shule hizo kuhusu masuala ya miundombinu, Jafo amesema “Sisi kama serikali hatutaki mtoto akose elimu hasa katika kipindi hichi ambacho serikali imeamua kuelekeza nguvu za kutosha kwenye elimu kwa ajili ya watanzania.”


Ameongeza “Kwa mzazi ambaye mtoto wake atabainika hajaenda shule na kupewa kazi zingine kama kuendesha bodaboda hatua za kisheria zichukuliwe mara moja,”.



 Pamoja na hayo, Jafo amekemea tabia ya wazazi kutotilia mkazo masuala ya elimu na kuwakabidhi watoto wao kuendesha bodaboda kama ajira yao badala ya kuwapeleka shule na kuwataka kuhakikisha wanawanunulia mahitaji yote ya shule.



Aidha amesema serikali haitarajii kuna vijana waliochaguliwa wakishawishiwa na wazazi kufanya vibaya kwenye mitihani kutokana na elimu kuwa ni bure.



Akizungumzia kuhusu watoto walioandikishwa kuanza kusoma elimu ya awali na msingi, Jafo amesema kumekuwepo na mwitikio mkubwa katika suala la uandikishaji watoto hao na linatokana na uwepo wa elimu bure.



Hata hivyo, amesema shule nyingi idadi ya wanafunzi imeongezeka zaidi na kwa serikali ni faraja kuona watanzania wengi sasa wanapata elimu huku akiwataka wazazi wahakikishe watoto walioandikishwa wanahudhuria shule ipasavyo  na wakurugenzi kuendelea kuweka mazingira bora ya kujifunzia na kufundishia.



Kadhalika, Jafo ameridhishwa na ukarabati wa miundombinu mbalimbali kwenye shule hizo huku akiwaahidi walimu kuwa serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufundishia ili waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi.
 

Naye, Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma, Godwin Kunambi, amesema kwasasa Manispaa hiyo inaendelea kukabiliana na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja ujenzi wa shule za msingi na sekondari na kuongeza madarasa kwenye baadhi ya shule ili kukabiliana na ongezeko la wanafunzi hasa wanaohamia Dodoma.



Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI) Seleman Jafo akipokea taarifa za maendeleo ya ujenzi wa madarasa shule ya msingi Chang’ombe ‘A’ kutoka kwa Afisa mteule daraja la -I-  ambaye ni Fundi mkuu kutoka (JKT) Aluleyani Mapunda wakati alipofanya ziara ya kukagua ujenzi wa madarasa shule ya msingi  hiyo unaofanywa katika kata ya Chang’ombe mjini Dodoma.

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Selemani Jafo akipokea maelekezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma  Godwin  Kunambi juu ya ukamilishaji ujenzi wa choo cha walimu shule ya msingi Chang’ombe ‘B’ pia uendelevu wa ujenzi wa vyoo vya wanafunzi  katika ziara yake aliyoifanya katika kata ya Chang’ombe.

No comments

Powered by Blogger.