Header Ads

Profesa MAKAME MBARAWA akemea Hujuma kwenye Miundo Mbinu ya Barabara SINGIDA

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa amewaagiza viongozi wa Serikali kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama na wananchi mkoani Singida kuwabaini na kuwachukulia hatua za kisheria wananchi wanaohujumu miundombinu ya barabara na kuisababishia hasara Serikali.

Profesa Mbarara ametoa agizo hilo mara baada ya kukagua ujenzi wa barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya yenye urefu wa Kilomita 89.3 kwa kiwango cha lami na kubaini kuwa baaadhi ya wananchi wameanza kuhujumu barabara hiyo.

“Tumepanga kujenga barabara ya Mkiwa-Itigi-Makongolosi kwa kiwango cha lami, sasa kitendo cha kuanza kuhujumu barabara iliyokwisha kamilika ni kitendo kisichokubalika na hatua kali zitachukuliwa kwa wote watakaobainika”, amesema Prof. Mbarawa.

Prof. Mbarawa amesisitiza umuhimu wa kila mwananchi wa Mkoa wa Singida na Tanzania kwa ujumla kuilinda miundombinu ya barabara, reli na mawasiliano ambayo inajengwa kwa fedha nyingi ili idumu kwa muda mrefu.

“Tutaimarisha stesheni ya Itigi na kuimarisha mawasiliano ya simu ili kuwezesha eneo hili kuwa na mawasiliano ya uhakika na kuchochea ukuaji wa uchumi wa mkoa wa Singida”, amesisitiza Waziri Prof. Mbarawa.

Meneja wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Singida Eng. Leonard Kapongo akimuonesha Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa uharibifu wa barabara unaotokana na ajali za barabarani katika barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya yenye urefu wa Kilometa 89.3mkoani Singida.
Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Prof. Makame Mbarawa, akihutubia wananchi wa Itigi mara baada ya kukagua barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya yenye urefu wa Kilomita 89.3 mkoani Singida, ambayo ujenzi wake kwa kiwango cha lami umekamilika kwa asilimia 98.

Katika hatua nyingine, Waziri Prof. Mbarawa amekagua ujenzi wa mzani wa kupima magari katika eneo la Bumbuwa katika yabarabara ya Manyoni-Itigi-Chaya na kumtaka Meneja wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS) Mkoa wa Singida Eng. Leonard Kapongo kuhakikisha ujenzi wa mzani huo unakamilika kwa wakati na magari yote yanayostahili yanapimwa.

Naye Meneja wa TANROADS Mkoa wa Singida Eng. Leonard Kapongo amemhakikishiaProf. Mbarawakuwa ujenzi wa barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya yenye urefu wa kilomita 89.3 umekamilika kwa asilimia 98 na umehusisha makalvati makubwa 48 madogo 118.

Zaidi ya shilingi bilioni 109.6 zimetumika katika ujenzi wa barabara ya Manyoni-Itigi-Chaya iliyojengwa katika mfumo wa usanifu na ujenzi ambayo ni sehemu ya barabara kuu ya Manyoni-Itigi-Chaya-Nyahua hadi Tabora.

No comments

Powered by Blogger.