Header Ads

Wafanyabiashara Kutoka Nchini Kongo Watakiwa Kutumia Bandari ya Dar es Salaam

Na Beatrice Lyimo-MAELEZO

Gavana wa Jimbo la Katanga katika Jamhuri ya Kidemokrasia Kongo (DRC) Jean Claude Kazembe ametoa wito kwa wananchi na wafanyabiashara kutoka nchini DRC kutumia Bandari ya Dar es Salaam kwa kuwa imeimarisha utoaji wa huduma kwa wateja.

Gavana Kazembe ametoa wito huo leo jijini Dar es salaam wakati wa ziara yake iliyolenga kudumisha uhusiano uliopo baina ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia Kongo.

“Awali kulikuwa na changamoto kadha wa kadha katika bandari ya Dar es salaam, ambapo kumekuwa na milolongo mingi wakati wa kupokea mizigo na kutozwa kwa kodi mbalimbali ikiwemo uhifadhi wa mizigo” alisema Gavana Kazembe.

Alisema kuwa uwepo wa dirisha la pamoja kwa mteja kuhudumiwa mahitaji yote sehemu moja kumerahisisha utendaji kazi bandarini hapo na kuondoa usumbufu kwa wafanyabiashara kutoka nje ya Tanzania.

Aidha, alisema kuwa kwa sasa mizigo ya DRC inashughulikiwa kwa haraka na hata kodi mbalimbali zilizokuwa zinatozwa zimepunguzwa, hivyo haoni sababu kwa wananchi wa DRC kukimbia bandari ya Tanzania.

Kwa upande wake Meneja Mawasiliano kutoka Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) Janeth Ruzangi amesema kuwa, Mamlaka imekamilisha mradi mpya wa Intergrated Security System (ISS) wenye CCTV camera 486 zenye uwezo wa kuona kila kitu kinachoendelea ndani ya bandari.

Janeth alisema kuwa Mamlaka imeanzisha Ofisi Lubumbashi kwa lengo la kuwasogeza zaidi wafanyabiashara wa DCR ambapo imerahisisha zaidi mchango na huduma zitolewazo kwa wateja wao.

No comments

Powered by Blogger.