Wafadhili Waridhishwa na Ukaushaji wa Mboga Mboga wa Wanawake Mkoani MOROGORO
Mkurugenzi wa mawasiliano wa taasisi ya
Mfuko wa Wanawake Afrika, Anna Salado (kulia), akipakua mboga zilizopikwa
kiasili na kuungwa kwa nazi wakati yeye na ujumbe wake walipotembelea mradi wa
ukaushaji wa mboga na matunda wa wanawake wa Kata ya Mzinga mkoani Morogoro
hivi karibuni. Kushoto
ni Naibu Meya wa Manispaa ya Morogoro, Milikieli Mansweat Mahiku.
Mratibu wa mradi wa Green Voices kutoka
taasisi ya Mfuko wa Wanawake Afrika ya Hispania, Alicia Cebada, akiwa
ameshikilia pakiti ya kisamvu kilichokaushwa na kufungashwa huku akiwapongeza
wanawake wa kikundi cha Mzinga katika Kata ya Mzinga, Manispaa ya Morogoro
kwamba wamefanya kazi nzuri sana. Mwenye fulana nyeupe ni Bi. Esther Muffui,
mshiriki kiongozi wa mradi huo.
SIYO tu mapishi ya
asili ya kisamvu kikavu kilichoungwa kwa nazi, lakini mafanikio makubwa katika
ukaushaji na usindikaji wa mboga na matunda katika mradi wa wanawake wa Kata ya
Mzinga, Manispaa ya Morogoro yamewavutia wahisani wa taasisi ya Women for
Africa Foundation kutoka Hispania.
Hali hiyo imewafanya
wanawake hao wawe katika nafasi kubwa zaidi ya kusonga mbele ikiwa wafadhili
hao watatoa tena fedha katika awamu ya pili ya mradi wa Green Voices unaotekelezwa
nchini Tanzania.
Akizungumza katika
Kijiji cha Konga kwenye Kata hiyo, mratibu wa mradi huo kutoka Hispania, Bi.
Alicia Cebada, alisema kwamba licha ya kuwa na muda mfupi tangu kuanza kwa
mradi huo, lakini wanawake hao wamefanya mambo makubwa ambayo yanastahili
kuungwa mkono.
“Hii teknolojia ya
ukaushaji wa mboga na matunda ni rahisi na inafaa sana kwa uhifadhi wa chakula,
kinachotakiwa ni kwa wanawake hawa kuwezeshwa zaidi,” alisema Alicia ambaye
aliongozana na Mkurugenzi wa habari wa taasisi hiyo, Anna Salado, na ofisa
mwandamizi wa taasisi hiyo anayeshughulikia masuaa ya ubunifu, Bi Noellia pamoja na mratibu wa Green Voices Tanzania,
Bi. Secelela Balisidya.
Alicia alisema kwamba,
changamoto ndogo wanazokabiliana nazo wamezisikia, lakini akasema katu
zisiwakatishe tamaa kwa sababu inaonyesha dhahiri wanaweza kufanya mambo
makubwa mbele ya safari.
Maofisa wa taasisi ya Mfuko wa Wanawake
Afrika kutoka Hispania wakiwa katika picha ya pamoja na wanakikundi wa Mzinga
(wenye sare). Kulia
ni mratibu wa mradi wa Green Voices nchini Tanzania, Bi. Secelela
Balisidya.
Mshiriki kiongozi wa kikundi cha Mzinga
Women Group, Esther Muffui (wa pili kushoto), akitoa maelezo ya namna ya
kukausha matunda katika mradi wa Green Voices kwenye Kata ya Mzinga mjini
Morogoro.
Post a Comment