Header Ads

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yaridhishwa na Bandari ya Tanga kupokea Mafuta

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Waziri  anayeshughulikia masuala ya Mafuta na Gesi wa DRC, Profesa Ngoyi Mukena wakipeana mikono mara baada ya kikao kilichofanyika jijini Tanga na kuhudhuriwa pia na Wataalam kutoka nchi hizo mbili.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Profesa Justin Ntalikwa (wa kwanza kushoto) na Mkurugenzi Msaidizi katika Idara ya Sheria, Wizara ya Nishati na Madini, Anna Ngowi (wa kwanza kulia) wakiwa katika kikao na  Waziri  anayeshughulikia masuala ya Mafuta na Gesi wa DRC, Profesa Ngoyi Mukena kilichofanyika jijini Tanga na kuhudhuriwa pia na Wataalam kutoka nchi hizo mbili.

Watendaji mbalimbali kutoka Serikali ya Tanzania wakiwa katika kikao na  Waziri  anayeshughulikia masuala ya Mafuta na Gesi wa DRC, Profesa Ngoyi Mukena kilichofanyika jijini Tanga na kuhudhuriwa pia na Wataalam kutoka nchi hizo mbili. Wa kwanza kulia ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Dkt. Mhandisi Juliana Pallangyo, wa kulia ni Kaimu Kamishna wa Nishati na Maendeleo ya Petroli, James Andilile.

............

Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) imeeleza kuridhishwa kwake na uwezo wa Bandari ya Tanga ambayo itatumika kupokea mafuta yatakayosafirishwa na Bomba la Mafuta kutoka Hoima nchini Uganda.

Hayo yamethibitishwa wakati wa kikao baina ya Waziri wa Nishati na Madini wa Tanzania, Profesa Sospeter Muhongo na Waziri  anayeshughulikia masuala ya Mafuta na Gesi wa DRC, Profesa Ngoyi Mukena kilichofanyika jijini Tanga na kuhudhuriwa pia na Wataalam kutoka nchi hizo mbili.

Waziri huyo na ujumbe wake walifanya ziara katika Bandari hiyo baada ya DRC kuonesha nia ya kusafirisha mafuta yake kwa Bomba hilo la Mafuta linalotoka Uganda hadi Tanga baada ya kugundua Mafuta katika Ziwa Albert ambapo itakuwa ikisafirisha mapipa 30,000 hadi Laki moja kwa siku.

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alisema kuwa Ujumbe huo utarudisha taarifa hiyo nzuri kwa Serikali ya nchi yao, aliongeza kuwa DRC wameahidi kuwashauri wafanyabiashara wa DRC kuendelea kuitumia Bandari ya Tanga na Dar es Salaam kwa shughuli za usafirishaji mafuta.

Pia, Waziri Muhongo alisema kuwa, Ujumbe huo umepata fursa ya kutembelea eneo la Chongoleani ambako inatarajiwa kujengwa gati itakayotumika kupakia mafuta ghafi kwenye Meli baada ya kutoka Hoima nchini Uganda, ambapo pia walitembelea Bohari za kuhifadhi mafuta ya kampuni ya GBP na kueleza kuwa, wafanyabiashara wa Kongo wataendelea kutumia huduma za kampuni hiyo.

Mbali na kuonesha nia ya utumiaji wa Bandari ya Tanga, Ujumbe wa DRC ulifika jijini Tanga kwa lengo la kuomba Serikali hizo mbili kushirikiana katika utafiti na uchimbaji wa  mafuta na gesi  Ziwa Tanganyika.

Katika Kikao hicho Mawaziri hao walikubaliana kuwa,  Wataalam wa pande mbili wanaosimamia Sekta hiyo wakutane kwanza kwa lengo la kufahamishana taarifa mbalimbali za Ziwa Tanganyika kuhusu  rasilimali za gesi na mafuta.

Vilevile, Profesa Muhongo alieleza kuwa, baada ya Wataalam wa pande zote kukutana, kitafuata kikao cha Mawaziri wa Sekta husika    kwa ajili ya kuweka  makubaliano ya namna ya kuendelea na utekelezaji wa shughuli za utafiti na  uchimbaji wa mafuta  Ziwa Tanganyika.

Kwa upande wake Waziri Mukena alikubaliana na mapendekezo ya Prof. Muhongo kuhusu Wataalam wa DRC na Tanzania kukutana na kujadili  taarifa za Ziwa Tanganyika zitakazosaidia kutekeleza suala la utafiti wa mafuta na gesi kwenye Ziwa hilo.

No comments

Powered by Blogger.