Header Ads

Mradi wa GREEN VOICES umeonesha Mafanikio Katika Kuwakomboa Wanawake TANZANIA


Makamu wa Rais mstaafu wa Hispania na Rais wa Taasisi ya Women for Africa Foundation, Mama Maria Tereza Fernandez de la Vega, akisalimiana na maofisa wa ulinzi na usalama mara baada ya kuwasili katika bandari ya Nansio, Ukerewe hivi karibuni kuzindua mradi wa kilimo cha viazi lishe unaofadhiliwa na taasisi yake ya inayoshughulikia maendeleo ya Wanawake wa Afrika.

Mama Getrude Mongella (waliosimama katikati mwenye blauzi nyekundu) akifafanua jambo kwa Mkamu wa Rais mstaafu wa Hispania na Rais wa Taasisi ya Women for Africa Foundation, Mama Maria Tereza Fernandez de la Vega, wakati walipotembelea mradi wa kilimo cha viazi lishe wilayani Ukerewe. Kushoto kwa Mama Mongella ni Bi. Leocadia Vedastus, ambaye ni mshiriki kiongozi wa mradi huo.

Makamu wa Rais mstaafu wa Hispania na Rais wa Taasisi ya Women for Africa Foundation, Mama Maria Tereza Fernandez de la Vega, akiangalia bidhaa zilizo mbele yake ambazo zinatokana na viazi lishe katika kuongeza mnyororo wa thamani. Hii ni wakati alipokwenda kuuzindua mradi huo wilayani Ukerewe katika Mkoa wa Mwanza.

MRATIBU wa mradi wa akinamama wapambanao na mazingira wa Green Voices, Alicia Cebada, amesema kwamba wamefarijika na mradi huo kwa kuwa umeonyesha mafanikio makubwa nchini Tanzania.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha ziara yao ya kutembelea miradi mitano kati ya 10 inayotekelezwa na wanawake wa Tanzania,hivi karibuni mratibu huyo kutoka taasisi ya Women for Africa Foundation, alisema hawakutegemea kama miradi waliyoianzisha akinamama hao ingeweza kufanikiwa katika kipindi kifupi tangu kuwapatia mafunzo.

“Ni kipindi kifupi tangu wanawake hawa walipopatiwa mafunzo nchini Hispania, lakini kwa hakika miradi waliyoibuni imeonyesha mafanikio, ni endelevu, rafiki wa mazingira na italeta tija kwao na taifa kwa ujumla,” alisema Alicia.

Aidha, alieleza kwamba, changamoto pekee ambayo ipo mbele yao ni kuhakikisha miradi hiyo inasimama na kuwafundisha wanawake wengi kadiri wawezavyo ili kuhakikisha wanajiletea maendeleo katika maeneo yao kiuchumi na kijamii.

“Tumewaona wanawake wa Ukerewe wanavyolima viazi lishe na kuongeza mnyororo wa thamani, tumewaona wanawake wa Kijiji cha Kitanga huko Kisarawe wakiongozwa na ‘Malkia wa Muhogo’ Abia Magembe, tumewatembelea akinamama wanaofuga nyuki kupambana na ukataji wa misitu huko Kisarawe, pia tumewaona wanawake wa Morogoro namna wanavyokausha mboga na kuwa na uhakika wa akiba ya chakula, na hapa (Bunju) tumeshuhudia jinsi kilimo cha uyoga kilivyo na faida, ni miradi mizuri, endelevu na rafiki mkubwa wa mazingira,” alisema.

No comments

Powered by Blogger.