Mradi wa GREEN VOICES umeonesha Mafanikio Katika Kuwakomboa Wanawake TANZANIA
Makamu wa Rais mstaafu wa Hispania na Rais
wa Taasisi ya Women for Africa Foundation, Mama Maria Tereza Fernandez de la
Vega, akisalimiana na maofisa wa ulinzi na usalama mara baada ya kuwasili
katika bandari ya Nansio, Ukerewe hivi karibuni kuzindua mradi wa kilimo cha
viazi lishe unaofadhiliwa na taasisi yake ya inayoshughulikia maendeleo ya
Wanawake wa Afrika.
Mama Getrude Mongella (waliosimama katikati mwenye blauzi nyekundu) akifafanua jambo kwa Mkamu wa Rais mstaafu wa Hispania na Rais
wa Taasisi ya Women for Africa Foundation, Mama Maria Tereza Fernandez de la
Vega, wakati walipotembelea mradi wa kilimo cha viazi lishe wilayani Ukerewe. Kushoto kwa Mama Mongella ni Bi. Leocadia Vedastus, ambaye ni mshiriki kiongozi wa mradi huo.
Makamu wa Rais mstaafu wa Hispania na Rais
wa Taasisi ya Women for Africa Foundation, Mama Maria Tereza Fernandez de la
Vega, akiangalia bidhaa zilizo mbele yake ambazo zinatokana na viazi lishe katika kuongeza mnyororo wa thamani. Hii ni wakati alipokwenda kuuzindua mradi huo wilayani Ukerewe katika Mkoa wa Mwanza.
MRATIBU wa mradi wa akinamama wapambanao na mazingira wa Green
Voices, Alicia Cebada, amesema kwamba wamefarijika na mradi huo kwa kuwa
umeonyesha mafanikio makubwa nchini Tanzania.
Akizungumza wakati wa kuhitimisha ziara yao ya kutembelea
miradi mitano kati ya 10 inayotekelezwa na wanawake wa Tanzania,hivi karibuni
mratibu huyo kutoka taasisi ya Women for Africa Foundation, alisema
hawakutegemea kama miradi waliyoianzisha akinamama hao ingeweza kufanikiwa
katika kipindi kifupi tangu kuwapatia mafunzo.
“Ni kipindi kifupi tangu wanawake hawa walipopatiwa mafunzo
nchini Hispania, lakini kwa hakika miradi waliyoibuni imeonyesha mafanikio, ni
endelevu, rafiki wa mazingira na italeta tija kwao na taifa kwa ujumla,”
alisema Alicia.
Aidha, alieleza kwamba, changamoto pekee ambayo ipo mbele yao
ni kuhakikisha miradi hiyo inasimama na kuwafundisha wanawake wengi kadiri
wawezavyo ili kuhakikisha wanajiletea maendeleo katika maeneo yao kiuchumi na
kijamii.
“Tumewaona wanawake wa Ukerewe wanavyolima viazi lishe na
kuongeza mnyororo wa thamani, tumewaona wanawake wa Kijiji cha Kitanga huko
Kisarawe wakiongozwa na ‘Malkia wa Muhogo’ Abia Magembe, tumewatembelea
akinamama wanaofuga nyuki kupambana na ukataji wa misitu huko Kisarawe, pia
tumewaona wanawake wa Morogoro namna wanavyokausha mboga na kuwa na uhakika wa
akiba ya chakula, na hapa (Bunju) tumeshuhudia jinsi kilimo cha uyoga kilivyo
na faida, ni miradi mizuri, endelevu na rafiki mkubwa wa mazingira,” alisema.
Post a Comment