Header Ads

YANGA, POLISI KOMBAINI KUCHEZA JUMAMOSI TAIFA.

images (2)
 
Na Frank Geofray-Jeshi la Polisi.
 
Timu Kombaini ya Polisi Tanzania na Yanga, Jumamosi hii zitacheza mchezo wa kirafiki katika uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam ili kujiweka sawa katika mashindano yanayowakabili ambapo Yanga inajiandaa kushiriki kombe la Kagame na Kombaini ya Polisi inajiandaa kushiriki katika michezo ya Umoja wa Wakuu wa Majeshi ya Polisi kusini mwa Afrika (SARPCCO) itakayoanza mwishoni mwa mwezi huu nchini Swaziland.
 
 Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mkuu wa kitengo cha Michezo wa Jeshi la Polisi, Jonas Mahanga amesema kikosi cha Polisi kitatumia mchezo huo kubaini mapungufu  na kuyafanyia marekebisho kabla ya kuelekea nchini Swaziland ambapo alisema taratibu zote zimeshakamilika.
 
Alisema Mchezo huo utakuwa mzuri na wa kuvutia kutokana na wachezaji wanaounda  kombaini ya Polisi kuonyesha kiwango kikubwa katika kambi yao inayoendelea katika Chuo Cha Taaluma ya Polisi(DPA) kilichopo kurasini jijini Dar es Salaam.
 
Mahanga alisema kombaini ya Polisi inaundwa na wachezaji Askari kutoka timu za Polisi za Tanzania bara na Zanzibar ambapo wengi wa wachezaji hao ni wale waliokuwa wanacheza ligi kuu ya bara na Zanzibar pamoja na ligi daraja kwanza.
 
Aidha Mahanga alisema kwa Upande wa Timu ya Mpira wa Pete nayo itacheza mchezo wa kirafiki na Kombaini ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania ili kuhakikisha kuwa inafanya vizuri nchini Swaziland na kurudi na ubingwa.
 
Alisema kwa ujumla timu zote zinazojiandaa na michezo hiyo zinaendelea vizuri ambapo Wanariadha waliokuwa katika kambi ya Taifa mkoani Manyara wiki hii wataungana na wenzao ili kufanya mazoezi kwa pamoja.
 
Lengo la Michezo hiyo ya SARPCCO  ni kujenga mahusiano miongoni mwa Askari Polisi wa nchi za kusini mwa Afrika pamoja na kubadilishana mbinu za kukabiliana na uhalifu ambapo Polisi Tanzania itashiriki katika mchezo wa mpira wa miguu, pete, riadha na vishale.

No comments

Powered by Blogger.