Header Ads

Waziri Profesa MAKAKE MBARAWA aiagiza TAA kuongeza Mapato yake

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa ameiagiza Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kuongeza kiwango cha ukusanyaji mapato kutoka Bilioni 74 hadi kufikia bilioni 105 katika mwaka wa fedha 2016/2017.

Ametoa agizo hilo jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na wafanyakazi wa Mamlaka hiyo mara baada ya kukagua majengo matatu na ofisi mbalimbali zilizopo Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. Julius Nyerere (JNIA).

Amesisistiza wafanyakazi wa Uwanja huo kuhakikisha kiasi cha ukusanyaji wa mapato hayo kinaongezeka siku hadi siku ili kukuza uchumi wa taifa na kuchochea fursa za kimaendeleo.

“Ni lazima muongeze kasi ya kufanya kazi ili mapato yaongezeke kwa kuwa uwezo mnao na nimeona kwenye viwanja vyenu kuna sehemu nyingi za biashara, hivyo mna kila sababu ya kukusanya kiasi hicho cha fedha”, amesema Prof. Mbarawa.

Aidha, katika ziara hiyo Waziri Prof. Mbarawa alibaini ucheleweshwaji wa vibali kwa abiria wanaoingia katika Uwanja wa Ndege wa  JNIA ambapo abiria huchukua zaidi ya saa moja kupata vibali.

“Nimesikitishwa na kitendo cha ucheleweshwaji wa vibali kutoka Idara ya Uhamiaji na huduma za kibenki zinazotolewa… hali hii haileti picha nzuri kwa wageni wetu. Abiria kuwekwa zaidi ya saa moja akisubiri kupata huduma, sitaki kuona hali hiyo ikiendelea”, amesisitiza Prof. Mbarawa.

Muonekano wa Jengo la Tatu (Terminal III) la abiria ambapo ujenzi wake unaendelea.
Sambamba na hilo amezitaka taasisi zote zinazofanya kazi katika viwanja vya ndege kushirikiana kwa ukaribu ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na kuongeza mapato kwa taifa.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Eng. George Sambali amemhakikishia Waziri Prof. Mbarawa kuwa mapungufu yaliyobainishwa yatafanyiwa kazi ili kuongeza ufanisi na huduma bora kwa abiria.

“Kwa kushirikiana na taasisi zote ambazo zinafanya kazi katika Kiwanja hiki tutahakikisha tunatoa huduma nzuri na kuongeza ufanisi katika utendaji ili kufikia malengo”, amesema Eng. Sambali.


Waziri Prof. Mbarawa amefanya ziara ya siku moja katika Kiwanja cha JNIA ili kuona utendaji kazi na maendeleo ya Ujenzi wa Jengo la Tatu la abiria ambapo jengo hilo linatarajiwa kukamilika mwezi Desemba 2017 na litakuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya abiria milioni sita kwa mwaka.

No comments

Powered by Blogger.