Header Ads

Serikali kushirikiana na Korea ya Kusini Kuendeleza Sekta za Habari ,Michezo na tasnia ya filamu

Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye akizungumza na ujumbe kutoka Korea ya Kusini ofisini kwake jijini Dar es Salaam kuhusu uwekezaji katika sekta ya Habari, Michezo na Utengenezaji wa Filamu nchini Septemba 23, 2016.
Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye akipokea zawadi ya jezi maalum kutoka kwa Mkurugenzi wa Klabu ya Soka ya Seongnam Bw. Suk Hoon Lee kutoka Korea ya Kusini, jezi hiyo ni zawadi maalum kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli kutoka kwa klabu hiyo Septemba 23,2016 jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye akiangalia zawadi ya kitabu aliyoipokea kutoka kwa Mkurugenzi wa TCN kutoka Korea ya Kusini Bw. Soon Young-Soon Septemba 23,2016 jijini Dar es Salaam.

.................
Na Raymond Mushumbusi WHUSM

Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau kutoka Korea ya Kusini wamekubaliana kushirikiana kuendeleza sekta za Habari, Michezo na filamu kwa kuwekeza katika miundombinu na wataalamu.

Pande hizo mbili zimekubaliana kushirikiana katika sekta hizo katika kikao kilichojumuisha ujumbe kutoka Kampuni ya TCN na Klabu ya Soka ya Seongam kutoka Korea Kusini na ujumbe kutoka Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo walipokutana leo Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali ya Tanzania, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Nape Moses Nnauye amesema kuwa kuja kwa ujumbe huo kutoka Korea ya Kusini ni fursa nzuri kwa Tanzania kuendeleza sekta za Habari, Michezo na Filamu kupitia wadau mbalimbali na wawekezaji kutoka nje ya nchi ambapo Serikali ipo tayari kushirikiana nao katika kuleta ufanisi na maendeleo katika sekta hizo.

“Ni matumaini yangu kuwa mazungumzo haya yataleta matunda kwani tayari tumeshazungumza nao kuhusu fursa zilizopo na kilichobaki ni wao kutuandikia rasmi ili tuanze sasa mchakato na matunda yataanza kuonekana hivi karibuni” Alisema Nnauye.

Aidha Mkurugenzi wa Klabu ya Soka ya Seongnam Bw. Suk Hoon Lee kutoka Korea ya Kusini amesema klabu yake ipo tayari kuwekeza katika shule ya michezo kwa vijana ili kuongeza kasi ya maendeleo ya soka kwa vijana.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa TCN kutoka Korea ya Kusini Bw. Soon Young-Soon alisisitiza kuwa kampuni yake imejiandaa kuja Tanzania kuwekeza katika utengenezaji wa Filamu kwa kuleta wataalamu na kutengeneza miundombinu ya kisasa katika utengenezaji wa filamu bora na utengenezaji wa vipindi mbalimbali nchini.

Naye Mkurugenzi wa Huduma za Redio kutoka Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) Suzana Mungy ameushukuru ujumbe kutoka Korea ya Kusini na kuahidi kuwapa ushirikiano wataalamu kutoka Korea ya Kusini na kuwakaribisha kuwekeza katika sekta ya Habari hasa utengenezaji wa vipindi bora.

Korea ya Kusini ni moja ya nchi rafiki wa Tanzania na kwa miaka mingi wamekuwa wakishirikiana katika sekta mbalimbali zikiwemo Habari, Michezo Utamaduni na Sanaa kwa ujumla.

No comments

Powered by Blogger.