Header Ads

Mfumo wa Usajili na Uhifadhi wa Takwimu za Matukio ya Binadamu Kuanzishwa, TANZANIA BARA

Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Maimuna Tarishi akitoa hatuba ya ufunguzi rasmi wa kikao cha wadau wa Usajili na Utunzanji wa Takwimu za Matukio Muhimu ya Binadamu nchini kilichofanyika katika ukumbi wa hoteli ya New Africa, Dar es Salaam.
Mtakwimu Mkuu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu Emilian Karugendo, akifafanua jambo wakati wa uwasilishaji wa mada iliyohusiana na hatua za kuandaa Mkakati wa Usajili na Uhifadhi wa Takwimu za Matukio Muhimu ya Binadamu wakati wa kikao cha wadau kilichofanyika katika ukumbi wa hoteli ya New Africa, Dar es Salaam.
Meneja wa Usajili kutoka RITA Angela Anatory akiwasilisha rasimu ya Mkakati wa Usajili na Uhifadhi wa Takwimu za Matukio Muhimu ya Binadamu katika kikao cha wadau kilichofanyika katika ukumbi wa hoteli ya New Africa, Dar es Salaam.
Mwakilishi wa Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa (WHO) Dkt. Rufaro Chatora akiongea kwa niaba ya wawakilishi wengine wa mashirika ya Umoja wa Mataifa waliohudhuria kikao cha wadau wa Usajili na Uhifadhi wa Takwimu za Matukio Muhimu ya Binadamu.
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dkt. Albina Chuwa akijibu baadhi ya maswali kutoka kwa wadau wakati wa kikao cha kujadili rasimu ya Mkakati wa Usajili na Uhifadhi wa Takwimu za Matukio Muhimu ya Binadamu katika ukumbi wa hoteli ya New Africa, Dar es Salaam.
....................................................... 

Na Veronica Kazimoto
 
Usajili wa Raia una jukumu la msingi katika kutekeleza matakwa ya utawala bora na maendeleo ya kiuchumi katika taifa lolote lile duniani.
 
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Sheria na Katiba Maimuna Tarishi wakati akifungua mkutano wa wadau wa kujadili Rasimu ya Mkakati wa Usajili na Uhifadhi wa Takwimu za Matukio Muhimu ya Binadamu uliofanyika jijini Dar es Salaam.
 
Tarishi amesema Usajili wa Raia ni wajibu wa kisheria kwa kuwa unasaidia katika upangaji wa mipango madhubuti ya maendeleo pamoja na kuiletea maendeleo jamiii kulingana na Mkakati wa Kuondoa Umaskini na Kukuza Uchumi Tanzania (KUKUTA II).
 
Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Katiba na Sheria amebainisha kuwa mfumo wa Usajili wa Raia uliopo sasa Tanzania Bara umekuwa ukifanya kazi kwa kusuasua na hivyo kusababisha baadhi ya wananchi kutotambulika katika kumbukumbu rasmi za kiutawala.
 
“Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi iliyofanyika mwaka 2012, ni asilimia 15 tu ya watanzania ndio waliosajiliwa na kupata vyeti, hali inayowaacha wengi pasipo kutambulika popote katika kumbukumbu rasmi za kiutawala,” amesema Tarishi.
 
Ameongeza kuwa usajili ya vifo ndio uko katika hali mbaya zaidi ambapo ni matukio machache ya vifo yanayoandikishwa na sababu za vifo hivyo hazibainishwi kwa usahihi au hazibainishwi kabisa hali inayosababisha ugumu katika kutekeleza majuku kwa upande wa sekta ya afya nchini.
 
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Dkt. Albina Chuwa ambaye ofisi yake ni mdau muhimu wa mfumo huu, amesema lengo la mkakati huu ni kuanzisha mfumo wa Usajili wa Raia ambao unakidhi vigezo vya kimataifa ambao ni wa kudumu na unaofikia watu wote katika kusajili matukio muhimu ya binadamu na kuzalisha takwimu za matukio hayo katika namna ambayo ni endelevu na ya kuaminika.
 
Dkt. Chuwa amesema mfumo huu wa Usajili wa Raia ukikamilika utasaidia kupata huduma zote za usajili katika sehemu moja kwa vituo vyote vya usajili nchini.
 
Nae Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili, Udhamini na Ufilisi (RITA) Emmy Hudson amesema mfumo uliopo sasa uko mbali na wananchi walio wengi hasa wa maeneo ya vijijini kwasababu ngazi ya chini ya usajili ni ofisi ya  Katibu Tawala wa Wilaya.
 
Changamoto hii na nyingine inasababisha huduma hii ya usajili kutofika kwa urahisi kwa wananchi walio wengi hali ambayo inaleta uhitaji wa mabadiliko ambayo ili tufanikiwe, RITA inahitaji peke yake haitamudu kuzikabili changamoto za mfumo pasipo kuhusisha wadau mbalimbali katika kuboresha mfumo huu.
 
Usajili wa Raia ulianzishwa na sheria ya kikoloni mnamo mwaka 1917. Kwa mujibu wa sheria hiyo usajili ulikuwa ni lazima kwa wakazi wa Tanganyika na baada ya uhuru, sheria hii ilirithiwa ambapo licha ya mabadiliko kadhaa ambayo yamekuwa yakifanyika bado wananchi wamekuwa na kasumba ya kutokuona umuhimu wa Usajili wa Raia nchini.

No comments

Powered by Blogger.