Header Ads

Waziri Mkuu KASSIM MAJALIWA azindua Mradi wa Uboreshaji Huduma za Umeme Jijini Dar es Salaam

 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, (katikati) na viongozi wengine kutoka kushoto, Mwenyekiti wa bodi ya TANESCO, Dkt. Alexander Kyaruzi, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Dkt. Juliana Palangyo,Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, (Waziri Mkuu), Waziri wa Biashara na Maendeleo wa Finland, Kai Mykkanen, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,  Paul Makonda na Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Felchesmi Mramba, wakishangilia baada ya kukata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa kituo cha udhibiti na usimamizi wa mifumo ya usambazaji umeme katika jiji la Dar  es salaam kilichoko Mikocheni jijini Dar es Salaam, leo Novemba 16, 2016.



.................................................

WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Mh. Kassim Majaliwa, amezindua kituo cha udhibiti na usimamizi wa mifumo ya usambazaji umeme katika jiji la Dar  es salaam kilichoko Mikocheni jijini Dar es Salaam, leo Novemba 16, 2016.

Kituo hicho kipya na cha kisasa, kimejengwa kwa ufadhili wa serikali ya Norway na Tanzania, chini ya mpango wa Mradi wa Uboreshaji Miundombinu ya Umeme jijini.

“Serikali ya awamu ya Tano, iliwaahidi Watanzania, wakati tukiomba kura, ya kwamba, tutaboresha huduma ya umeme kote nchini, na leo hii ni ushahidi tosha tunatekeleza kwa vitendo ahadi zetu.” Alisema Waziri Mkuu ambaye alimwakilisha Rais wa Tanzania, Mh. Dkt. John Pombe Magufuli.

Akimkaribisha waziri Mkuu, Waziri wa Nishati na Madini, Mh. Profesa Sospeter Muhongo amesema, watanzania wanahitaji umeme tena ulio bora, na sasa kituo hicho ni jawabu la kuwapatia umeme ulio bora.

“Kati ya vitu ambavyo sitarajii kuvisikia ni mgao wa umeme, lakini pia bei ya umeme, kuusu bei tutakaa, pembeni na watu wa TANESCO kulizungumzia hili. “ Alitoa hakikisho Waziri Muhongo.

Kwa upande wake, Waziri wa Biashara na Maendeleo wa Finland, Mh. Kai Mykkanen, alisema, teknolojia iliyotumika kwenye mitambo ya kituo hicho ni ya kisasa ijulikanayo kama Distribution SCADA System, na inauwezo wa kutambua hitilafu ya umeme kwa haraka na hivyo kurahisisha kurekebisha hitilafu hiyo kwa wakati.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Felchesmi Mramba, alisema, Mradi wa uboreshaji huduma za umeme jijini Dar es Salaam ulibuniwa kwa lengo la kuboresha miundombinu ya umeme katika jiji la Dar es Salaam kutokana na ongezeko kubwa la mahitaji ya umeme katika sekta za kiuchumi hususan katika maeneo ya katikati ya jiji, Kariakoo, Ilala na maeneo ya wilaya ya Kinondoni.

Alisema, utekelezaji wa mradi huu umehusisha ujenzi wa kituo cha kupoza nguvu za umeme chenye ukubwa wa 100MVA (2X50MVA), 132/33KV cha City Centre, ujenzi wa mfumo wa njia ya usafirishaji umeme chini ya ardhi (Underground Transmission Line) na kwa kutumia minara (Overhead Line) ya msongo wa wa kilovolti 132 kutoka kituo cha Ilala hadi kituo cha City Centre umbali wa Kilomita 3.4, vile vile ujenzi wa mfumo wa njia ya usafirishaji umeme chini ya ardhi, (Underground Transmission Line) kutoka kituo cha Makumbusho hadi kituo cha City Centre umbali wa kilomita 6.67.

“Mheshimiwa Waziri Mkuu, kituo hiki ambacho kinajulikana kitaalamu kama Distribution SCADA System kitawezaesha watoa huduma wetu kufuatilia kwa haraka zaidi pale matatizo ya umeme yanapojitokeza kwa kutumia mifumo ya ksiasa ya kompyuta.” Alifafanua Mhandisi Mramba na kuongeza.

“Nia hasa ni kujenga vituo vingine kama hiki kwa kuanza na miji mingine mikubwa ya Arusha, Mwanza, Mbeya na Dodoma.” Alisema.

 Waziri Mkuu na wageni wengine wakitembelea chumba cha mitambo yaudhibiti na usimamizi wa mifumo ya usambazaji umeme Distribution SCADA System.

 Waziri Mkuu akitembeela moja ya mitambo inayopatikana kwenye kituo chicho (Server).

 Mtaalam wa mitambo, wa shirika la Umeme Nchini Tanzania, (TANESCO), Bi, Mwajua Turkey, kushoto, akimpatia maelezo waziri mkuu wakati akitembelea kituo hicho muda mfupi kabla ya kukizindua rasmi.

 Waziri Mkuu akitoa hotuba yake.

 Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, akitoa hotuba yake.

 Waziri wa Biashara na Maendeleo wa Finland, Mh. Kai Mykkanen.

Waziri Mkuu, akifungua kitambaa kuashiria uzinduzi huo.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, (wapili kushoto), Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, (wapili kushoto), Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, Dkt. Juliana Palangyo, (kushoto) na Waziri Kai(kulia), wakishangilia baada ya uzinduzi.

No comments

Powered by Blogger.