Siku ya Takwimu AFRIKA yafanyika Jijini Dar es Salaam
Emmanuel
Ghula, Dar
es Salaam
Wizara, Idara, Wakala,
Taasisi za Serikali, Mashirika yasiyokuwa ya Serikali na Wadau wa Maendeleo wametakiwa kutumia takwimu zinazotolewa na
Ofisi ya Taifa ya Takwimu katika kupanga na kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo
hapa nchini.
Akizungumza katika
Maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika leo jijini Dar es Salaam Naibu Katibu
Mkuu wa Wizara ya Fedha, Prof. Adolf Mkenda amesema kuwa matumizi ya takwimu
bora ndio msingi katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo.
“Leo tunasherehekea Siku
ya Takwimu Afrika, siku ambayo inatukumbusha umuhimu wa Takwimu katika
utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya taifa letu. Ukiwa na takwimu bora utaweza
kutoa huduma zilizo bora,” amesema Prof. Mkenda.
Prof. Mkenda amesema uwepo
wa takwimu bora zinazoonesha mahitaji halisi ya wananchi ndio dira katika
utaoji wa huduma muhimu za kila siku pamoja na upangaji na utekelezaji wa
miradi mingine ya maendeleo ya kitaifa.
“Maadhimisho haya leo
yanazitaka Serikali zetu kuimarisha mifumo ya kitakwimu kwa kuwekeza katika
teknolojia ya kisasa ya ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa Takwimu. Serikali
kwa upande wake itahakikisha inaiwezesha Ofisi ya Taifa ya Takwimu kuwekeza
katika teknolojia ya kisasa zaidi ili iweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo
ya ukusanyaji wa Takwimu bora na kwa wakati,” amesisitiza Prof. Mkenda.
Kwa upande wake
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Dkt. Albina Chuwa amesema Siku ya
Takwimu Afrika kwa mwaka huu imelenga katika kuufahamisha umma kuhusu umuhimu
wa Takwimu bora kwa maendeleo yao na Taifa kwa ujumla.
“Siku hii ya Takwimu
Afrika ni muhimu sana kwetu sisi hasa watakwimu kwani tunaitumia kuelimisha
umma juu ya umuhimu wa Takwimu katika mustakabali wa maendeleo ya Taifa,”
amesema Dkt. Chuwa.
Dkt. Chuwa amesema kupitia
maadhimisho haya yanayoongozwa na kauli mbiu ya "Takwimu Bora kwa Maisha
Bora", itawasaidia wananchi kutambua kuwa uwepo wa takwimu bora ndio njia
ya upatikanaji wa maendeleo stahiki.
Nae Mkuu wa Kitengo
cha Teknolojia Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kutoka Mamlaka ya Usimamizi na
Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), Dkt. Carina Wangwe amesema wakiwa
kama watumiaji wakubwa wa Takwimu zinazotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu
katika utekelezaji wa majukumu yao ndio wanathamini mchango wa takwimu rasmi katika
kupanga mipango ya maendeleo.
“Sisi ni wadau wakubwa
na watumiaji wa takwimu zinazotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu, leo hii tupo
hapa ili kushirikiana na ofisi hii ili kuhakikisha teknolojia ya kisasa
inatumika katika uboreshaji wa Takwimu na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma
mbalimbali kwa jamii,’ amesema Dkt. Wangwe.
Siku ya Takwimu Afrika
huadhimishwa tarehe 18 Novemba, kila mwaka, Kwa hapa Tanzania maadhimisho haya yamefanyika
Novemba 23, 2015 ambapo kauli mbiu ya maadhimisho hayo kwa mwaka huu ni “Takwimu
Bora kwa Maisha Bora".
Post a Comment