Header Ads

KENYA, UGANDA zaimarisha hali ya Usalama

Uganda na Kenya zimeimarisha usalama kufuatia mashambulio yaliyotekelezwa mjini Paris mwishoni mwa wiki, kuzuia mashambulio kutoka kwa wapiganaji wa Kiislamu.

Msemaji wa polisi nchini Uganda amesema polisi na wanajeshi wameimarisha doria kuzuia mashambulio, hasa kutoka kwa wapiganaji wa Kiislamu wa al-Shabaab kutoka Somalia.

“Kama tahadhari, tumeimarisha usalama na kiwango chetu cha tahadhari na pia tukaongeza maafisa wa usalama. Kuna maafisa wa usalama saa 24 katika maeneo yenye watu wengi,” Bw Enanga alinukuliwa na gazeti la serikali la New Vision.

Nchini Kenya, usalama pia umeimarishwa mpakani na katika miji mikuu, gazeti la kibinafsi la Standard limeripoti.

Polisi zaidi walitumwa Jumapili kulinda makanisa na maduka makubwa pamoja na maeneo yenye kukusanyika watu wengi, gazeti hilo linasema.

Mwandishi wa BBC David Wafula amewapata maafisa wa Vijana wa Huduma kwa Taifa (NYS) wakitumiwa kukagua watu wanaoingia katika maduka ya jumla.

"Tunapondelea kuimarisha doria, tunawataka wananchi pia wawe macho,” mkuu wa polisi Joseph Boinnet amesema.

Al-Shabab waliua watu 150 waliposhambulia Chuo Kikuu cha Garissa mwezi Aprili mwaka huu na watu 67 katika shambulio jumba la kibiashara la Westgate jijini Nairobi mwaka 2013.
Nchini Uganda, mashambulio mawili ya al-Shabab mwaka 2010 yaliua watu 70.

No comments

Powered by Blogger.