Header Ads

Mkurugenzi Mpya wa Idara ya Habari Maelezo huyu Hapa

Na Shamimu Nyaki-WHUSM

Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Nape Moses Nnauye amemtangaza  Bw.Hassan Abbas kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO  na Msemaji Mkuu wa Serikali  kuanzia Agosti 5 Mwaka huu.

Uteuzi huo umefanyika kwa mujibu wa Sheria za Utumishi wa Umma Namba 8 ya mwaka 2002 kifungu Namba 6(1)(b) kufuatia uhamisho wa aliyekuwa Mkurugenzi wa Idara hiyo Bw. Assah Mwambene uliofanyika  tarehe 7 Machi 2016 kwenda Wizara ya Mambo ya Nje na  Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mhe.Nape Moses Nnauye ametoa wito kwa Wanahabari na Wananchi  kwa ujumla kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Bw Abbas atakapokuwa anatekeleza majukumu yake.

“Ninawaomba Wanahabari na Watanzania kwa ujumla mumtambue Bw Abbas na mtoe ushirikiano unaostahili katika utendaji wa kazi zake”.Alisema Mhe. Waziri.

Aidha Mhe. Waziri Nape alimpongeza Bibi Zamaradi Kawawa aliyekuwa anakaimu nafasi hiyo kwa  kujituma na kusimamia majukumu yote ya Idara kwa ukamilifu na uadilifu.

Kwa upande wake Mkurugenzi huyo mpya amekubali uteuzi huo na ameahidi kuitumikia nafasi hiyo kwa uadilifu mkubwa na ameomba ushirikiano wa kutosha kutoka kwa wafanyakazi wa Idara ya Habari Maelezo na Watanzania kwa ujumla.

Kabla ya uteuzi huo Bw. Hassan Abbas  alikuwa ni Meneja Habari na Mawasiliano katika Ofisi ya Rais inayosimamia Utekelezaji wa Program ya Matokeo Makubwa sasa (President`s Delivery Bureau).

Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali Bw.Hassan Abbas(kushoto) akizungumza na waandishi wa habari(hawapo pichani) mara baada ya kutangazwa kushika nafasi hiyo leo Agosti 9,2016 katika ukumbi wa Wizara Jijini Dar es Salaam katikati ni Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Nape Moses Nnauye na kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari MAELEZO Bibi. Zamaradi Kawawa.

No comments

Powered by Blogger.