Header Ads

TAKUKURU YAKANUSHA TUHUMA ZA RUSHWA DHIDI YA NAPE

Steven Chami, Kamanda wa Takukuru mkoa wa Lindi


*Yasisitiza hiyo ni michezo michafu ya kisiasa.
*Yavitaka vyombo vya habari kuwa makini
Na Mwandishi Wetu. Lindi
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Lindi imekanusha tuhuma rushwa dhidi ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM Ndugu Nape Nnauye zilizoandikwa na baadhi ya magazeti ya leo.
Akizungumza na waandishi wa habari nje ya Ofisi yake, Kamanda wa Takukuru mkoa wa Lindi Ndugu Steven Chami amefafanua kuwa kilichofanywa jana ilikuwa ni kujiridhisha na viwango vya fedha vinavyotolewa na wanasiasa wote walioomba ridhaa ya kugombea nafasi mbalimbali mkoani humo.
Ndugu Chami alisema Ndugu Nape ni miongoni mwa wanasiasa wanaoomba ridhaa ya ubunge kupitia CCM katika jimbo la Mtama mkoani Lindi na kwamba kwa kuwa alikuwa ni miongoni mwa wanasiasa aliyeingia katika benki ya NMB mjini Lindi jana ili kutoa fedha ilikuwa si jambo la busara kuacha aende bila kujiridhisha na kiwango pamoja na matumizi ya fedha husika alizokuwa akichukua.
Hata hivyo Kamanda huyo wa TAKUKURU alisisitiza kuwa baada ya kumuomba Ndugu Nape kuongozana naye ofisini kwake kwa mahojiano ambayo yalichukua kati ya dakika 30 na 45, alijiridhisha kuwa kiwango cha fedha alichokuwa amechukua benki ni cha kawaida.
Kwa mujibu wa Kamanda huyo wa TAKUKURU, Ndugu Nape alichukua benki jumla ya shilingi Milioni Tatu ambazo alitaka kuzitumia kwa ajili ya kuwalipa Mawakala wake 156 ambao aliwaandaa kusimamia zoezi la upigaji kura katika vituo vyote jimboni humo, na kwamba kiasi hicho cha fedha kilikuwa pungufu hata ya uhalisia wa mahitaji yake.
Ndugu Chami amevitaka vyombo vya habari kuwa makini katika kuripoti habari zake na kuepuka upotoshaji kama huo uliofanywa na magazeti ya leo ya Nipashe, Mtanzania, Majira na Tanzania Daima jambo ambalo linajenga dhana inayobeba dhamira na malengo mabaya dhidi ya mtu au taasisi.
Alisisitiza kuwa kuna baadhi ya wagombea ambao wamekamatwa na maafisa wake na kwamba uchunguzi unaendelea na kwamba mara utakapokamilika watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma za rushwa zinazowakabili na kwamba Ndugu Nape sio miongoni mwao kwa sababu yeye hakukamatwa akitoa wala kupokea rushwa.

No comments

Powered by Blogger.