Header Ads

Taasisi za Serikali Ziwe Tayari Kutumia Mtandao Mmoja wa Mawasiliano

OM1
Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue akifungua mkutano wa Serikali Mtandao unaowahusisha Makatibu Wakuu, Makatibu Tawala,Wakurugenzi, Watendaji Wakuu wa Taasisi na Wakala za Serikali unaofanyika katika Ukumbi wa AICC leo jijini Arusha.
 
OM2
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Vijana,Utamaduni na Michezo Sihaba Nkinga akifuatilia mada mbalimbali wakati wa Mkutano Mkuu wa mwaka wa Serikali Mtandao ngazi ya Makatibu Wakuu, Makatibu Tawala, Wakurugenzi na Watendaji wakuu wa Taasisi za Serikali unaoendelea jijini Arusha.
 
OM3
Baadhi ya washiriki wa Mkutano wa Mwaka wa Serikali Mtandao wakifuatilia mkutano huo leo jijini Arusha.
 
OM4
Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Makatibu wakuu, Makatibu Tawala wa mikoa,Wakurugenzi wa Halmashauri na Watendaji wa Taasisisi mbalimbali za Serikali mara baada ya kufungua Mkutano wa Serikali Mtandao leo jijini Arusha.
 ...................................................
 
 
Na Aron Msigwa -Arusha

Serikali imezitaka Wizara,Idara,Wakala na Taasisi  mbalimbali kuanza kujiandaa na mageuzi makubwa ya matumizi ya Mfumo mmoja wa  Mawasiliano kupitia Serikali Mtandao ili kupunguza gharama za uendeshaji na kuondoa urudufu wa mifumo ya TEHAMA inayofanya kazi za aina moja serikalini.

Hatua hiyo ya Serikali imekuja kufuatia kuwepo kwa mifumo ya TEHAMA ya kutolea huduma kwa umma katika Taasisi mbalimbali za Serikali isiyoweza kuwasiliana na kubadilishana taarifa jambo linalosababisha usumbufu kwa wanannchi wanapotakiwa kuwasilisha taarifa za aina moja kwenye taasisi tofauti za serikali.

Akifungua Mkutano wa Serikali Mtandao wa Makatibu Wakuu,Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakurugenzi na Watendaji Wakuu wa Taasisi na Wakala za Serikali leo jijini Arusha Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amesema kuwa mabadiliko hayo ni Sehemu ya mpango wa Serikali wa kuhakikisha kuwa  inawafikishia wananchi huduma bora kwa haraka, gharama nafuu na mahali walipo.

Ameeleza kuwa hatua ya Tanzania kuweka msukumo kwenye Serikali Mtandao haiepukiki kwa kuwa imelenga kuboresha utendaji wa kazi ndani ya Serikali, kuongeza tija, ufanisi na kasi ya ubadilishanaji wa taarifa ndani ya Serikali.

"Jambo hili la Serikali mtandao tumeshalizungumza sana Serikalini kutokana na umuhimu wake tumekutana watoa maamuzi kwa mara ya kwanza ili kufikia malengo ya Serikali mtandao tuliyojiwekea kila mmoja achukue hatua kuhakikisha kuwa fursa zilizopo zinatumika ipasavyo,tumeshaanza hakuna kurudi nyuma katika jambo hili" 

Amesema Serikali imefanya mageuzi makubwa katika uwekezaji wa miundombinu ya TEHAMA ikiwemo uanzishaji wa Mkongo wa Taifa, Kituo cha Taarifa Serikalini (National Data Centres) ili kuhakikisha kuwa huduma za Serikali zinapatikana kwa urahisi, haraka,uwazi,gharama nafuu,wakati wowote na mahali popote nchini.

"Serikali tumefanya uwekezaji mkubwa kwenye miundombinu ya TEHAMA ikiwemo Mkongo wa Taifa (NICTBB), Mtandao wa Serikali (GovNet),Vituo vya kitaifa vya Data na kutenga  Masafa ya Intaneti ya Serikali, hii yote ni kuwahakikishia wananchi huduma bora za Serikali mtandao"  Amesisitiza Balozi Sefue.

Amefafanua kuwa Serikali imeendelea kuboresha Sera na sheria, kutokana kutungwa kwa Sera ya TEHAMA ya mwaka 2003 na Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Serikali Mtandao 2013 pamoja na sheria ya Elekroniki na Mawasiliano ya Posta (Elektonic and Postal Communicatins),Sheria ya Miamala ya Kielektroniki 2015 na Sheria ya Makaosa ya Mitandao ya mwaka 2015.

Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kujenga uwezo wake wa ndani ili kuondoa utegemezi wa wakandarasi wa nje katika ujengaji wa mifumo ya TEHAMA hapa nchini ambao huigharimu serikali fedha nyingi.

"Tunalo jukumu kubwa la kuhakikisha tunaimarisha na kujenga uwezo wetu wa ndani ili kuondoa utegemezi kutoka nje, wataalamu sasa tunao na tutaendelea kujenga uwezo wetu wa miundombinu ya ndani ili kuwahudumia wananchi"

Ametoa wito kwa wataalam wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Tume ya Mipango na Wakala ya Serikali Mtandao kushirikiana katika kuhakikisha Serikali Mtando inaingizwa katika mpango wa taifa wa miaka mitano.

Aidha, amezitaka Taasisi ambazo zina kiwango kidogo cha utekelezaji wa Serikali mtandao kushirikiana na Wakala ya Serikali Mtandao kuchukua hatua za haraka ili kuhakikisha kuwa matumizi ya TEHAMA yanaleta ufanisi katika kujenga Serikali Mtandao madhubuti.

"Taasisi za Serikali ambazo bado zina kiwango kidogo cha utekelezaji wa Serikali Mtandao zinatakiwa kuchagua jambo moja, kukubali  kubadilika au kubadilishwa" amesisitiza na kuongeza kuwa Serikali inaendelea kuzijengea uwezo taasisi hizo ziweze kuendana na mabadiliko yaliyopo.


Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Arusha Bw.Felix Kijiko Ntibenda akiwakaribisha washiriki wa mkutano huo jijini Arusha amesema kuwa kufanyika kwa mkutano huo ni mwanzo mzuri wa kuelekea Serikali Mtandao Imara.

Amesema matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Serikali yameisaidia Serikali kuongeza ufanisi katika shughuli mbalimbali ikiwemo utambuzi, tiba, ukusanyaji wa mapato ya Serikali na huduma za matibabu.

Amesema kupitia mifumo ya ukusanyaji wa mapato kwa njia ya mtandao mkoa wa Arusha anaouongoza umenufaika kwa kiasi kikubwa kwa kuongeza mapato ya ndani na kufanikiwa kupunguza vitendo vya wizi na ubadhirifu.

Awali akizungumza kuhusu mkutano huo Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Serikali Mtandao (e Government Agency) Bw. Jabir Bakari amesema kuwa mkutano huo umelenga kuongeza ufanisi katika matumizi ya Rasilimali za TEHAMA nchini.

Amesema Serikali  inaendelea kufanya vizuri katika kufanikisha lengo kubwa la kufikisha huduma kwa wananchi pia kufanikisha mpango wa kuwa na mfumo mmoja utakaowezesha taarifa zote za wananchi kuwa katika sehemu moja.

 Kuhusu mkutano huo  Dkt.Jabiri amesema kuwa washiriki watapata fursa ya kujadili  masuala mbalimbali ya ushirikiano katika kutekeleza jitihada za Serikali Mtandao nchini pamoja na Kutafuta ufumbuzi wa changamoto za serikali mtandao zilizopo nchini ili kuleta  maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Aidha,amesema washiriki watapata fursa ya kujifunza kutoka kwa wataalam wengine wanaohusika na Serikali Mtandao kutoka nchi zinazofanya vizuri katika eneo la Serikali mtandao zikiwemo India na Singapore.

 Pia amesema mada mbalimbali zitajadiliwa zikiwemo za usimamizi wa Serikali Mtandao nchini Tanzania, Hali ya miundombinu  ya Serikali mtandao na Utekelezaji wa Mpango wa Uendeshaji wa Serikali kwa uwazi.

Mada nyingine zitahusu uimarishaji wa uwazi na Mfumo wa Takwimu huria nchini Tanzania na uimarishaji wa huduma za Serikali kupitia simu za mkononi na mifumo inayotumika kutoa huduma kwa wananchi.

No comments

Powered by Blogger.