Header Ads

Wananchi Jijini MBEYA Waendelea Kupatiwa Elimu Kuhusu JOTO ARDHI

xx2
Meneja Mkuu Shirika la Uendelezaji Nishati ya Jotoardhi Tanzania (TGDC), Mhandisi Boniface Njombe (aliyesimama) akielimisha Umma wa Kata ya Swaya wakati walipotembelea eneo la kata hiyo ikiwa ni sehemu ya Kampeni ya uelimishaji kuhusu manufaa ya Jotoardhi hivi karibuni mkoani Mbeya. Kushoto ni Mkurugenzi wa masuala ya Ufundi wa TGDC, Bwana Karamaeli Mnjokava.
 
xx4
Mkurugenzi wa masuala ya Ufundi wa TGDC, Bwana Karamaeli Mnjokava.(aliyesimama mbele) akichangia mada kuhusu jotoardhi na manufaa yake kwa wakazi wa Kata ya Swaya hivi karibuni mkoani Mbeya.

xx5 xx7
Baadhi ya Wakazi wa Kata ya Swaya pamoja na baadhi ya Watendaji wa Kampuni ya Uendelezaji Nishati ya Jotoardhi (TGDC) wakifuatilia uwasilishwaji wa mada toka kwa Meneja Mkuu wa TGDC hivi karibuni mkoani Mbeya.
………………………………………………………………………………….

Habari Picha na Benedict Liwenga, Maelezo-Mbeya.
 
Mkoa wa Mbeya unasemekana kuwa ni moja ya maeneo yaliyobarikiwa kuwa miongoni mwa maeneo ambayo Shirika la Uendelezaji wa Jotoardhi Tanzania (TGDC) linatarajia kuanza shughuli ya uchimbaji jotoardhi kutokana na tafiti za awali kuhusu nishati hiyo kuanza katika mkoa huo.
 
Kauli hiyo imetolewa na Meneja Mkuu wa TGDC, Mhandisi Boniface Njombe wakati wa Kampeni ya Uelimishaji kuhusu Jotoardhi kwa viongozi katika ngazi za Kata za Ilomba katika Vijiji vya Ituha, Tonya pamoja na Kata nyingine ya Nanyala iliyoko Mbozi Mkoani Mbeya.
 
Mhandisi Njombe amesema kuwa, TGDC ina malengo ya kuzalisha zaidi ya megawati 200 kwa mkoa huo licha ya mkoa huo kwa sasa kutumia megawati 40 jambo ambalo linaweza kupelekea nishati hiyo itakayozalishwa kupeleka katika mikoa mingine ya jirani kwani kiasi hiko cha umeme kitakuwa ni kikubwa.
 
Aidha, amewataka wakazi wa Mbeya kuonyesha ushirikiano kati ya Serikali yao pamojana TGDC ili zoezi hilo lenye manufaa kwao liweze kufikiwa kwa maendeleo ya mkoa na vijijini ambako kuna changamoto ya ukosefu wa nishati ya umeme pia kutatua tatizo la mgao wa umeme katika mkoa huo.
 
“Tuunge mkono jitihada hizi za Serikali ili walau nishati hii izidi kuendelezwa na ituokoe dhidi ya hali ya umeme isiyokuwa na uhakika kwani tukishakuwa na uelewa na kuelimisha wananchi na kutoa ushirikiano, tutakaa mkao wa kula kutokana na nishati hii”, alisema Njombe.
 
Kwa upande wake Mjiolojia Mwandamizi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, Bwana Jacob Mayalla ameeleza kuwa kutokana na juhudi za Serikali, tafiti za jotoardhi nchini zilizanza miaka ya 1976 hadi mwaka 1978 zikiwa kama tafiti za awali ambazo ziliweza kubainisha maeneo katika nchi ya Tanzania kwenye maeneo yaliyopitiwa na Bonde la Ufa ambapo viashiria vya jotoardhi vipo.
 
“Kwa Mkoa wa Mbeya, tafiti za jotoardhi zilifanywa na Serikali kwa kushirikiana na Wakala wa Jiolojia Tanzania”, alisema Mayalla.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa masuala ya Kiufundi toka  Kampuni ya TGDC, Bwana Taramaeli Mnjokava ameyataja baadhi ya matumizi ya moja kwa moja ya jotoardhi nchini ikiwemo matumizi ya kiutalii ambapo maji ya jotoardhi huwekwa kwenye mabwawa hivyo huvutia watalii wa ndani na nje ya nchi kwa kuyaoga na kuyaangalia jambo ambalo linaongeza pato la taifa.
 
Aliongeza kuwa, maji ya jotoardhi hufaa kwa matumizi ya uzalishaji wa samaki kwani samaki hupenda maji yenye hali ya uvuguvugu kuliko yenye baridi hasa kwa maeneo yenye baridi kama mkoa wa Mbeya, hivyo pindi mabwawa ya samaki yanapotengenezwa na kuwekewa maji ya jotoardhi yanasaidia kuzalisha samaki kwa wingi jambo ambalo nalo litakuza pato kwa taifa na kwa eneo husika ambalo uzalishaji unafanyika.
 
“Maji ya jotoardhi yanaweza kutumika katika uzalishaji wa mboga mboga au maua kwa njia ya Vitalu Nyumba kwa Kiingereza huitwa Green Houses lakini ni vitalu hutengenzwa kwa plastiki au kioo, hivyo watu hutumia vitalu hivi jambo ambalo linavutia sana soko la nje kwani huwa hawapendi mboga zilizopigwa dawa wala maua yaliyopigwa dawa, niwahamasishe kujiandaa kwa kuupokea mradi huu kwani utawanufaisha vyakutosha nyie wakazi wa Mbeya na taifa kwa ujumla,” alisema Mnjokava.
 
Mnamo tarehe 19 Disemba, 2013 Serikali ya Tanzania kupitia Shirika la Ugavi wa Umeme (TANESCO) ilisajiri kampuni ya kuendeleza nishati itokanayo na Jotoardhi, jina la kampuni likiitwa “Tanzania Geothermal Development Company Limited (TGDC).
 
Kampuni hii ilianzishwa kama kampuni tanzu ya Shirika la TANESCO ambalo linamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100 na mnamo mwezi Julai 2014 TGDC ilianza kazi zake rasmi ikipewa jukumu la kuharakisha uendelezaji wa nishati ya jotoardhi nchini.

No comments

Powered by Blogger.