Header Ads

Serikali yasisitiza Matumizi ya TEHAMA

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw.HAB Mkwizu (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Maendeleo ya Serikali Mtandao na malengo ya Serikali katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Serikali.Kulia ni Mkurugenzi wa Uwezeshaji wa Huduma za TEHAMA kutoka Wakala ya Serikali Mtandao. 
          
Na Aron Msigwa –Maelezo

Serikali imesema kuwa itaendelea kuboresha miundombinu yake ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kote nchini ili kuwawezesha wananchi  kupata huduma  mbalimbali  za Serikali kwa uwazi mahali walipo kupitia mtandao.

Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw.HAB Mkwizu wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Maendeleo ya Serikali Mtandao na malengo ya baadaye ya uimarishaji wa matumizi ya TEHAMA katika shughuli za Serikali.

Amesema ili kuimarisha uwazi na upatikanaji wa Takwimu huria,Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya TEHAMA kwa lengo la kuwawezesha wananchi kupata huduma zinazotolewa na Wizara na Taasisi za Serikali kupitia simu zao za mkononi mahali walipo.

Ameeleza kuwa ili kulinda na kuthamini mafanikio yaliyopatikana nchini Tanzania Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, kupitia Wakala ya Serikali Mtandao(e Government Agency) imeandaa Mkutano Mkuu wa mwaka wa wataalamu wa TEHAMA na Watendaji Wakuu wa Serikali utakaofanyika jijini Arusha kuanzia Agosti 17 hadi 20 mwaka huu.

Bw. Mkwizu amesema kuwa Mkutano huo utafunguliwa na Katibu Mkuu kiongozi Balozi Ombeni Sefue chini ya kauli mbiu isemayo Kaulimbiu ya Mkutano huo ni Uwezeshaji wa Wananchi kupitia TEHAMA.

 Amesema kuwa washiriki zaidi ya 500 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali zinazotoa huduma kwa umma watapata fursa ya kujadili  masuala mbalimbali ya ushirikiano katika kutekeleza jitihada za Serikali Mtandao nchini Tanzania, Kutafuta ufumbuzi wa changamoto zilizopo ili kuleta  maendeleo ya kiuchumi na  kijamii.

Amebainisha kuwa kupitia mkutano huo washiriki watazungumzia namna bora ya uimarishaji wa utoaji wa huduma kwa umma kupitia ushirikiano  wa maarifa na ukuzaji wa uhusiano wa kikazi.

Aidha, wataalam wa TEHAMA wa Tanzania watapata fursa ya kujifunza kutoka. Kwa  wataalam wengine wanaohusika na Serikali Mtandao kutoka nchi zinazofanya vizuri katika eneo la Serikali mtandao zikiwemo India na Singapore.

Bw.Mkwizu ameeleza kuwa wakati wa mkutano huo mada mbalimbali zitajadiliwa zikijikita  katika usimamizi wa Serikali Mtandao nchini Tanzania, Hali ya miundombinu  ya Serikali mtandao na Utekelezaji wa Mpango wa Uendeshaji wa Serikali kwa uwazi .

Mada nyingine zitahusu uimarishaji wa uwazi na Mfumo wa Takwimu huria nchini Tanzania na uimarishaji wa huduma za Serikali kwa wananchi kupitia simu za mkononi na mifumo inayotumika kutoa huduma kwa wananchi.

No comments

Powered by Blogger.