Header Ads

DED Chamwino apewa wiki mbili kukamilisha mradi wa maji Manzase

Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI Selemani Jafo akiwataka Viongozi wa Serikali kutumia vyema pesa za Mfuko wa Busket Fund ambao ni mfuko wa fedha za Afya katika kuimarisha huduma bora ya Afya nchini
 Naibu Waziri Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Selemani Jafo akikagua kifaa cha kisasa cha kupimia macho katika hospitali ya Mvumi wakati wa ziara yake ya kukagua huduma ya Hospitali Kimbizi inayohusisha Madaktari Bingwa ambao wanatibu magonjwa mbalimbali Wilayani Chamwino. Kampeni hiyo itadumu kwa muda wa siku tano kuanzia tarehe 15 Mei, 2017 hadi Mei 19, 2017
  
Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa TAMISEMI selemani Jafo akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa Serikali, Madaktari Bingwa, Viongozi wa Dini na Siasa katika Hospitali ya Mvumi.
....................................................................
Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI)Selemani Jafo amemtaka Mkurugenzi wa Wilaya ya Chamwino Athuman Masasi kuhakikisha kuwa Mradi wa maji wa kijiji cha Manzase unamalizika ifikapo mwishoni mwa mwezi mei, mwaka huu.

Jafo ameyasema hayo alipokuwa anafanya ziara yake katika hospitali ya Mvumi ambapo amezindua huduma ya Hospitali Kimbizi inayohudumiwa na Madaktari Bingwa ambao watatoa huduma ya kitabibu kwa siku tano kuanzia leo, tarehe 15 hadi Mei 19, 2017 wilayani humo.

Madaktari hao bingwa watatibu magonjwa ya ndani kwa watu wote, watoto, mifupa, masikio, pua na koo, meno, upasuaji na magonjwa ya uzazi kwa upande wa akinamama.

Mbali na hilo pia, amesema katika sehemu mbalimbali alizopita kumekuwa na changamoto ya kukosa huduma bora katika vituo vya Afya kutokana na urasimu walionao Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa na kufanya Wananchi wengi wasio na uwezo wa kupata huduma hizo katika kipindi cha nyuma na kwa kipindi  hiki Serikali imeshatoa ufumbuzi ambao Viongozi mnapaswa kuzitumia vyema pesa za Miradi ya Afya kama Busket Fund katika kuboresha huduma za Afya kwa Wananchi wote.

Aidha Jafo amewataka Wananchi kushiriki kikamilifu katika kupata huduma hizo kutoka kwa Madaktari bingwa waliotoka katika hospitali mbalimbali nchini kwani huduma hizo zinapatikana kwa bei nafuu na kutoka kwa Madaktari bingwa wenye uzoefu mkubwa na wa muda mrefu.

Amepongeza ushirikiano uliopo wa Mganga Mkuu wa Dodoma Dk.James Kiologwe Mbunge wa Jimbo la Mtera, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, wadau mbalimbali  pamoja na Kanisa la Anglikana kwa kuweza kuendesha zoezi hilo la huduma.


Akihitimisha hotuba yake iliyojaa maelekezo ya Serikali, Jafo amesema baada ya zoezi hili kukamilika ingependeza madaktari bingwa wote walioshiriki zoezi hili katika Wilaya zote za Dodoma waje kujipongeza mjini Dodoma na kuwa mfano bora wa kuigwa kwa kuwa zoezi hili ni zoezi la kwanza kufanyika nchini na likiwa limefanyika mkoani Dodoma.

No comments

Powered by Blogger.