Header Ads

Jamii yashauriwa Kushiriki Mazoezi ya Viungo vya Mwili ili Kujenga Afya Zao

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akiongoza matembezi ya mazoezi yaliyoanzia Tungamaa hadi Viwanja vya Mnazi mmoja Wete, huku akiwapungia mkono wananchi waliokuwa wamejipanga barabarani. 
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akishiriki matika kufanya mazoezi ya kunyoosha viungo katika Viwanja vya Mnazi mmoja Wete.
Baadhi ya vikundi vya mazoezi vikishiriki matembezi hayo ya mazoezi.
Vijana wa Brasband wakisherehesha matembezi hayo ya mazoezi.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akizungumza na wanavikundi wa mazoezi katika Viwanja vya Mnazi mmoja Wete.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akikabidhi zawadi ya vifaa vya mazoezi kwa mmoja kati ya wanamazoezi hao.
Na: Hassan Hamad (OMKR)
 
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, ameuthibitishia ulimwengu kuwa yuko katika afya njema, baada ya kuongoza matembezi ya mazoezi kwa zaidi ya kilomita sita.
 
Matembezi hayo yaliyoanzia eneo la Tungamaa hadi viwanja vya Mnazi mmoja Wilaya ya Wete, yamevishirikisha vikundi kadhaa vya mazoezi kutoka Mkoa wa Kaskazini Pemba.
 
Akizungumza baada ya matembezi hayo, Maalim Seif amesema yuko vizuri na anaweza kutembea kwa mazoezi mara mbili zaidi ya neo hilo alilotembea.
 
Ametoa wito kwa wananchi wa Zanzibar kushiriki katika mazoezi ili kuimarisha afya zao, kwani mazoezi ni sehemu ya tiba mbadala kwa maradhi mbali mbali yakiwemo sukuri, presha na maumivu ya viungo.
 
Amefahamisha kuwa wananchi wengi waliojiunga na vikundi vya mazoezi wakiwa na matatizo hayo tayari wamepata nafuu, na sasa hawapendi tena kuacha kufanya mazoezi kwani kufanya hivyo ni kukaribisha maradhi yasiyokuwa na ulazima.
 
Aidha Maalim Seif ameitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo kuandaa programu za kuyatangaza mazoezi nchini, ili wananchi waweze kushajiika zaidi kufanya mazoezi.
Amesema nchi nyingi duniani ikiwemo uchina, zimekuwa zikishajiisha mazoezi kwa watu wa rika zote wakiwemo vikongwe, hali inayosaidia kulinda afya za wananchi hao na kupunguza gharama za matibabu.
 
Katika kuunga mkono mazoezi hayo, Makamu huyo wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ametoa zawadi ya vifaa vya michezo kwa baadhi ya vikundi vya mazoezi katika Mkoa huo, na kuahidi kuchangia vifaa zaidi kwa makundi mengine yaliyobakia.
 
Nae Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Mhe. Said Ali Mbarouk, amempongeza Maalim Seif kwa ujasiri wake wa kushajiisha wananchi kufanya mazoezi, hali inayotoa mwamko kwa wananchi wengi kuanza kufanya mazoezi.
 
Amesema baada ya Makamu wa Kwanza wa Rais kuzindua vikundi vya mazoezi katika Jimbo la Gando mwezi April mwaka huu, kisiwa cha Pemba kilikuwa na vikundi 30 vya mazoezi, lakini ndani ya kipindi cha miezi minne vimeongezeka kufikia vikundi 60.
 
Ameeleza kuwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo itaendelea kushirikiana na vikundi vya mazoezi ili kuona kuwa hali ya mazoezi inakwenda vizuri, na kuwawezesha wananchi wengi zaidi kuweza kushiriki.
 
Mapema akisoma risala ya vikundi hivyo vya mazoezi nd. Omar Dadi amesema wamefarajika baada ya Makamu wa Kwanza wa Rais kutekeleza ahadi yake na kushiriki katika matembezi hayo ya mazoezi.
 
Amesema utaratibu wa kufanya mazoezi umewasaidia sana wananchi wa Kisiwa cha Pemba kiafya, na kuwashauri wananchi wengine kuanza kufanya mazoezi bila kujali shughuli na umri walionao.

No comments

Powered by Blogger.